MATUKIO MATANO YALIYO BAMBA MECHI YA YANGA VS SIMBA OCTOBER 1, 2017 LEO NINI KITATOKEA?

 Tokeo la picha la mashabiki wa simba na yanga image

Mara Nyingi mechi ya Simba na Yanga huacha matukio ya kukumbukwa kwenye soka la bongo kutokana na ukubwa wa mechi husika unaosababishwa na historia ya timu hizi mbili kongwe kwenye anga la michezo la Tanzania zilizoanzishwa kabla hata ya uhuru wa Tanganyika.
 
Kwenye mchezo wa Yanga vs Simba uliochezwa October 1, 2016 na kumalizika kwa sare ya kufungana goli 1-1, kuna mambo mengi sana yalijiri kwenye mechi ile ambayo yameacha alama itakayodumu siku zote.
 
 https://www.kiungomshambuliaji.blogspot.com inakuletea matukio matano (5) yaliyotikisa ndani ya dakika 90 kutoka kwenye mechi ya Yanga vs Simba iliyopita.

1. GOLI LA AMIS TAMBWE.

Ni goli ambalo lilizua sintofahamu uwanjani na kupelekea mchezo kusimama kwa dakika kadhaa wakati wachezaji wa Simba wakimzonga mwamuzi kuhoji uhalali wa goli hilo ambapo walikuwa wanadai Tambwe aliushika mpira kabla ya kufunga.
 
Tambwe alifunga goli hilo akipokea pasi ndefu iliyopigwa kutoka katikati ya uwanja, wakati anaumiliki mpira, uligusa mkono wake kabla ya kumpita beki wa Simba Novalty Lufunga kisha mrundi huyo kumchambua golikipa wa Simba wakati huo Vicent Ang’ban na kuweka gozi nyavuni.

2. VURUGU ZA MASHABIKI.

Baada ya Tambwe kufunga goli kwa upande wa Yanga, ambalo mashabiki wa Simba walitafsiri halikuwa goli halali, wakaanza kufanya vurugu wakipinga uamuzi wa mwamuzi Martin Saanya kulikubali goli hilo.
 
Mashabiki wa Simba walianza kung’oa viti na kuvitupa chini, ilibidi polisi kutumia mabomu ya machozi  kudhibiti vurugu hizo ambazo awali zilianzia nje ya uwanja ambapo mashabiki wa timu zote walivunja mageti wakati wa kuingia uwanjani kwa sababu ya wingi wao huku mashine za kieletroniki zikishindwa kwenda na kasi ya wingi wa watu

3. KADI NYEKUNDU YA JONAS MKUDE.

Mwamuzi wa mchezo huo Martin Saanya alimtoa nje kwa kadi nyekundu nahodha wa Simba Jonas Mkude lakini haikueleweka mara moja sababu ilikuwa ni nini kwa sababu Mkude alionekana kubishana kwa ukali kwa muda  mrefu na mwamuzi pengine ikadhaniwa huenda alimtolea lugha chafu.
 
Lakini katika mabishano kati ya Mkude na Saanya (mwamuzi) pamoja na baadhi ya wachezaji wa Simba, mwamuzi alionekana kuyumba na kuanguka chini kitendo kilichotafsiriwa huenda Mkude alihusika kwa namna moja au nyingine kwa mwamuzi huyo kuanguka.
 
Lakini baadae kamati ya saa 72 ilipitia malalamiko ya Simba kuhusu kadi nyekundu ya Mkude na baadhi ya makosa yaliyofanywa na mwamuzi Martin Saanya ambapo Mkude alifutiwa kadi nyekundu na Martin Saanya kuondolewa kwenye orodha ya waamuzi wanaochezesha mechi za ligi kuu Tanzania bara.

4. KUKATALIWA KWA GOLI LA AJIBU.
Ni miongoni mwa vitu vilivyozua mijadala mikubwa baada ya mchezo wa Simba na Yanga kumalizika, goli lililofungwa na Ajibu na kukataliwa lilionekana lilikuwa halali kwa mujibu wa picha za marudio za Azam TV.
 
Kutokana na uhalali wa goli hilo, mwamuzi wa pembeni  siku hiyo (line one) Samwel Mpenzu pia aliadhibiwa kwa kufungiwa kuchezesha mechi za ligi kuu Tanzania bara.

5. GOLI LA KUSAWAZISHA LA SHIZA KICHUYA.
Kichuya aliisawazishia Simba dakika za lala salama wakati Yanga wakiamini watatoka na ushindi wa goli 1-0 siku hiyo.
 
Kichuya alipiga kona kutoka Kaskazini Mashariki ya uwanja wa taifa na mpira kwenda moja kwa moja kwenye nyavu za Ali Mustafa ‘Barthez’ na kuiandikia Simba bao la kusawazisha.
 
Goli hilo lilimpa umaarufu mara dufu Kichuya na kuwafanya mashabiki wa Simba kumuona Kichuya ni mwokozi wao kutokana na bao lake ambalo liliwafanya Simba kukwepa kipigo cha tatu mfululizo kwenye mechi za ligi.
 
Je, nini kitajiri kwenye mechi ya Simba vs Yanga LEO February 25, 2017? Endelea kuwa karibu na https://www.kiungomshambuliaji.blogspot.com kujua matukio yatakayobamba ndani na nje ya uwanja.
Share on Google Plus

About KASSIM OMARY

HII NI BLOG AMBAYO ITAKUWA INAKUPA HABARI MOTOMOTO ZA KIMICHEZO NA HABARI KWA UJUMLA
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 Maoni:

Post a Comment