TFF YAITUPIA MBALI RUFAA YA KLABU YA POLISI DAR DHIDI YA SIMBA!

Tokeo la picha la TANZANIA FOOTBALL FEDERATION IMAGE

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), limepokea rufaa kutoka Klabu ya Polisi Dar es Salaam dhidi ya Klabu ya Simba kuhusu kumchezesha Mchezaji Novalty Lufunga katika mchezo wao wa Raundi ya Tano ya Kombe la Azam Sports Federation Cup 2017.
 
Madai ya Polisi ni kwamba Mchezaji Novalty Lufunga alioneshwa kadi nyekundu kwenye mchezo kati ya Simba na Coastal Union katika mchezo wa Azam Sports Federation Cup 2015/2016 uliofanyika Uwanja wa Taifa, Aprili 11, mwaka jana.
 
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limetupilia mbali rufaa hiyo kwa kukosa vigezo vya kikanuni katika uwasilishaji wake na hivyo kukosa sifa ya kusikilizwa. Hii ni kwa mujibu wa kanuni ya 18 (1) na (2) ya Kanuni za Kombe la Shirikisho la Azam Sports HD.
 
Kanuni ya 18 (1) inasema: “Malalamiko yoyote kuhusiana na mchezo yawasilishwe kwa maandishi kwa kamishna wa mchezo au TFF sio zaidi ya masaa sabini na mbili (72hrs) baada ya kumalizika mchezo.”
 
Kanuni ya 18 (2) inasema: Ada ya malalamiko ni shilingi laki tatu (Tshs 300,000.00). Malalamiko yo yote yatakayowasilishwa bila kulipiwa ada na kuwasilishwa nje ya muda uliowekwa hayatasikilizwa.”
 
Hata hivyo, Shirikisho linapenda kutoa ufafanuzi kuhusu kadi nyekundu aliyopewa Mchezaji Novalty Lufunga katika mashindano ya Azam Sports Federation Cup 2016/2017.
 
Kwa utaratibu wa mashindano haya ambayo ni ya mtoano, adhabu za kadi (njano na nyekundu) zitolewazo uwanjani, zinakoma mwisho wa msimu wa shindano husika isipokuwa kadi hizo zikiongezwa adhabu ya kinidhamu (suspension) ambayo itafahamisha kwa klabu na mchezaji kwa maandishi.
 
Kadhalika, Kanuni ya 16 ya Kanuni za Kombe la Shirikisho Sehemu ya Tatu inaeleza wazi kuwa matumizi ya kanuni za ligi zitahusika maeneo yanayoruhusu uendeshaji wa shindano la mtoano.
 
“Adhabu zote zinazohusisha katika mashindano ya Kombe la Shirikisho la Azam HD zitahusisha na shindano hili tu,” inasema kanuni ya 16 (3) na (4).
 
KAMBI YA KILIMANJARO WARRIORS
Timu ya Tanzania ya vijana wenye umri wa chini ya miaka 23 ‘Kilimanjaro Warriors’ inatarajiwa kuingia kambini Janauri 29, 2017 kwa ajili ya maandalizi ya awali ya kucheza mechi za kufuzu fainali za Olimipiki zitakazofanyika jijini Tokyo, Japan mwaka 2020.
 
Kambi hiyo ya wiki moja itafanyika kwenye Hosteli za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ambako pia kuna Uwanja wa Karume, Ilala jijini Dar es Salaam kwa ajili ya mazoezi kulingana na program za walimu.
 
Tanzania haijapata kushiriki Michuano ya Olimpiki kwa upande wa mpira wa miguu jambo ambalo limeisukuma TFF kuona kuwa ni fursa ya mpira wa miguu kuchezwa hivyo inashirikiana na Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), kufanikisha mipango na taratibu.
 
Tanzania kwa sasa ina vijana wengi waliotokana na michuano ya Mradi wa kuibua na kukuza vipaji wa Airtel kadhalika na Cocacola ambao wamekuwa chachu ya maendeleo ya timu ya taifa ya vijana wenye umri wa chini ya miaka 17 maarufu kwa jina la Serengeti Boys.
 
Vijana hawa wa Airtel, Copa Cocacola na Serengeti Boys wataungana na baadhi ya vijana waliofanya vizuri kwenye Ligi ya Vijana wenye umri wa chini miaka 20 kutoka timu za Ligi Kuu ambao wamezaliwa baada ya tarehe 1 Januari 1997 ili kuunda kikosi imara cha awali kuelekea kufuzu kwa michuano ya Olimpiki itakayofanyika Tokyo Japan, mwaka 2020.
 
Kwa kufuata utaratibu wa maandalizi ya Serengeti Boys na kwa kushirikiana na TOC timu hii itapewa mazoezi na michezo  ya kujipima nguvu ndani na nje ya nchi.
 
IMETOLEWA NA SHIRIKISHO LA MPIRA WA MIGUU TANZANIA (TFF)
Share on Google Plus

About KASSIM OMARY

HII NI BLOG AMBAYO ITAKUWA INAKUPA HABARI MOTOMOTO ZA KIMICHEZO NA HABARI KWA UJUMLA
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 Maoni:

Post a Comment